Comment

Topic

Ufahamu

Estimated reading: 6 minutes 106 views

Summary: Ufahamu ni dhana inayorejelea kujua na kulielewa jambo kwa usahihi na kuweza kulielezea upya kwa usahihi bila kupoteza maana yake ya msingi. Ufahamu wa mtu waweza kupimwa katika kusikiliza jambo au katika kusoma.

Ufahamu wa Kusikiliza

Ufahamu wa kusikiliza ni zaidi ya kusikiliza tu kile kilichosemwa. Badala yake, ni uwezo wa mtu kuelewa maana ya maneno anayoyasikia na kuweza kuhusiana nayo kwa namna fulani. Kwa mfano, mwanafunzi anaposikiliza hadithi, ufahamu mzuri wa kusikiliza humsaidia kuielewa hadithi hiyo, kuikumbuka, kuijadili, na hata kuisimulia tena kwa maneno yake mwenyewe.

Kujibu Maswali ya Ufahamu kutokana na Habari uliyoisikiliza

Ufahamu wa kusikiliza unahusisha michakato kadhaa katika kuelewa na kupata maana ya kile kinachozungumzwa. Michakato hii inahusisha:

  • Kuelewa vizuri sarufi ya lugha inayozungumzwa.
  • Kuelewa vyema maana ya maneno ya mhusika anayezungumza.
  • Kuelewa sintaksia (muundo wa maneno) ya sentensi kwa namna zinavyowasilishwa.

Katika ufahamu wa kusikiliza, msikilizaji hana budi kuzingatia mambo yafuatayo:

  1. Kuwa Makini: Elekeza akili yote kwa mzungumzaji ili kuweza kusikia kila anachokisema.
  2. Kutilia Maanani Vidokezo vya Maana: Bainisha iwapo msemaji anaongeza jambo jipya, anatofautisha, anafafanua au anahitimisha hoja.
  3. Kuandika Mambo Muhimu: Andika baadhi ya mambo unayoona kuwa ni ya muhimu ili kukusaidia kukumbuka hapo baadaye.
  4. Kuwa Makini na Ishara za Mwili: Ishara kama vile kurusha mikono, kutingisha kichwa, kutingisha mabega, au hata kupepesa macho zinachangia kwa kiasi kikubwa kupata maana katika mazungumzo.

Kufupisha kwa Mdomo Habari uliyoisikiliza

Ili kuweza kufupisha kwa mdomo habari uliyoisikiliza, mambo yafuatayo ni ya kuzingatia:

  1. Baini Mawazo Makuu: Bainisha mawazo makuu yanayopaswa kujitokeza katika habari iliyofupishwa.
  2. Panga Maelezo kwa Usahihi: Panga maelezo kwa usahihi katika usemaji.
  3. Kichwa cha Habari: Kichwa cha habari kinapaswa kihusiane na ufupisho na wazo kuu.
  4. Sema kwa Ufasaha: Sema ufupisho kwa ufasaha na kwa lugha nzuri.

Mfano

Fupisha kwa mdomo habari uliyoisikiliza.

Ufahamu wa Kusoma

Ufahamu wa kusoma ni ule mtu anaoupata kwa njia ya kusoma makala, kifungu cha habari, kitabu, au gazeti.

Kusoma kwa Sauti kwa Kuzingatia Lafudhi ya Kiswahili

Soma kwa sauti kwa kuzingatia lafudhi ya Kiswahili.

Vipengele vya Ufahamu wa Kusoma

Kuna vipengele viwili vinavyounda mchakato wa ufahamu wa kusoma:

  1. Uelewa wa Msamiati:
    Ili kuelewa habari/matini, ni lazima msomaji awe na uwezo wa kuelewa msamiati uliotumika katika matini hiyo. Endapo maneno yaliyotumika hayataeleweka, matini yote haitafahamika.
  2. Uelewa wa Matini:
    Katika ufahamu wa kusoma, msomaji anatakiwa kuzingatia mambo yafuatayo:
  • Kubaini mawazo makuu: Msomaji anaposoma habari fulani au kitabu inatakiwa ajiulize, “Je, kinachozungumziwa hapa ni nini? Ni jambo gani hasa analolizungumzia mwandishi?”
  • Kuzingatia alama za uakifishi: Hii itamsaidia kuelewa ujumbe wa habari hiyo na kuepuka kupotosha maana ya mwandishi.
  • Kubaini maana ya maneno na misemo mbalimbali: Habari nyingine zina maneno ya kisanaa, hivyo ni muhimu msomaji kubaini maana ya maneno hayo katika muktadha wa habari hiyo ili kuelewa vyema maana ya mwandishi.
  • Kumakinikia kile anachokisoma: Kila kipengele anachokisoma inampasa akielewe vizuri.

Kwa kuzingatia haya yote, msomaji atakuwa na uelewa mzuri juu ya habari aliyoisoma na pia anaweza kufupisha habari hiyo aliyoisoma.

Kujibu Maswali kutokana na Habari uliyoisoma

Ili kujibu maswali yanayotokana na habari uliyoisoma, inatakiwa kuzingatia mambo yafuatayo:

  • Kubaini mawazo makuu.
  • Kuzingatia alama za uandishi.
  • Kubaini maana ya maneno na misemo mbalimbali.
  • Kutilia maanani vidokezo vya maana.
  • Mawazo yanapaswa kuelekezwa katika jambo linalosomwa, kujiuliza maswali kadri unavyosoma na kuandika ufupisho.

Kufupisha Habari uliyoisoma

Ili kuandika ufupisho mzuri wa habari uliyosoma, yapaswa kuzingatia yafuatayo:

  • Kuisoma habari uliyopewa zaidi ya mara moja.
  • Kubainisha mawazo makuu.
  • Kuandika ufupisho kwa lugha fasaha na yenye mtiririko mzuri wa hoja.
  • Kuhesabu idadi ya maneno na kuhakikisha haizidi idadi inayotakiwa.
  • Kupitia habari ya mwanzo na kisha ufupisho ili kuona kama taarifa muhimu haijaachwa au kusahaulika.

Kusoma kwa Burudani

Huu ni usomaji ambao lengo lake kuu ni kujiburudisha. Katika usomaji wa aina hii, msomaji hujisomea zaidi magazeti, majarida, na vitabu tofauti na vile vinavyotumika darasani.

Wakati mwingine, sio lazima msomaji awe na vitabu vyote anavyohitaji kusoma. Inapotokea hivyo, msomaji anaweza kwenda maktaba kuazima kitabu anachokihitaji.

Ingawa lengo la msomaji ni kujiburudisha, hujiongezea maarifa. Hii ni kwa sababu magazeti, majarida, na vitabu, sambamba na kutumia lugha sanifu, huelezea mambo mbalimbali yanayohusu jamii.

Mambo ya Kuzingatia katika Ufahamu wa Kusikiliza

Msomaji kutokana na kusoma vitabu na majarida mbalimbali hujiongezea kiwango cha welewa wa lugha na mambo mengine ya kijamii yanayojadiliwa humo. Ni jambo zuri kwa msomaji kujijengea tabia ya kujipima ili aweze kuelewa kiwango cha maarifa aliyopata katika kujisomea.

Kujipima huku kunaweza kufanywa kwa kujiundia utaratibu wa kuweka kumbukumbu ya vitu au makala zilizosomwa na kufanya ufupisho wa kila makala.

Utaratibu wa Kujipima na Kuweka Kumbukumbu ya Usomaji wa Burudani:

  • Tarehe:
  • Jina la Kitabu/Makala/Gazeti:
  • Mchapishaji:
  • Mwaka/Tarehe ya Uchapishaji:
  • Ufupisho wa Habari (yasizidi maneno 20):
  • Fundisho/Ujumbe Mkuu:
  • Jambo Lililokuvutia Sana:
  • Maoni ya Jumla:

Matumizi ya Kamusi

Kamusi ni kitabu cha marejeo chenye msamiati uliokusanywa kutoka kwa wazungumzaji wa jamii fulani na kupangwa katika utaratibu maalumu, kisha kufafanuliwa kwa namna ambayo wasomaji wanaweza kuelewa. Kamusi pia inaweza kuwa orodha ya maneno yaliyo katika karatasi au nakala tepe yaliyopangwa kialfabeti na kutolewa maana pamoja na maelezo mengine na kuhifadhiwa katika kitabu, santuri, simu, tarakilishi au katika mfumo wowote wa kielektroniki.

Jinsi ya Kutumia Kamusi

Maneno yanayoingizwa katika kamusi hupangwa kwa utaratibu wa alfabeti. Maneno yanayoanza na herufi fulani yote huwekwa chini ya herufi hiyo. Maneno yanayoanza na herufi fulani nayo hupangwa katika utaratibu wa alfabeti kwa kuzingatia herufi ya pili, ya tatu, nne au tano ya neno kama mfano hapa chini unavyoonyesha:

Mfano:

ja, jabali, jabiri, jadhibika, jadi.

Maneno yote yanaanza na herufi [j]. Herufi ya pili kwa maneno yote ni [a]. Herufi ya tatu ni [b] na [d]. Kwa kuwa [b] hutangulia [d] katika mpangilio wa alfabeti, maneno yenye [b] huwekwa kabla ya yale yenye [d]. Kwa kuwa maneno yenye herufi [b] ni mawili, itabidi tutazame herufi ya nne ya maneno haya ili kuchagua litakaloorodheshwa mwanzo. Neno ‘jabali’ litaorodheshwa kabla ya ‘jabiri’ kwa kuwa [a] (herufi ya nne) ya ‘jabali’ hutangulia [i] ya ‘jabiri’ ambayo pia ni herufi ya nne. Kisha tunatazama maneno yenye [d] kama herufi ya tatu. Hapa pia tunatazama herufi ya nne ili kubaini neno litakaloandikwa mwanzo kati ya ‘jadhibika’ na ‘jadi’. Kwa kuwa [h] hutangulia [i], basi ‘jadhibika’ huorodheshwa mwanzo ndipo lifuatiwe na ‘jadi’.

Kwa hiyo, hivi ndivyo unavyopaswa kutafuta neno kwenye kamusi. Nenda kwenye herufi ya neno unalotafuta kisha litafute kwa kufuata mlolongo huo wa herufi ya kwanza, ya pili, na kadhalika.

Neno linaloorodheshwa kwenye kamusi ili lifafanuliwe linaitwa kidahizo. Kidahizo huandikiwa maelezo ya kukifafanua. Maelezo haya ni matamshi ya kidahizo, maana ya kidahizo, kategoria ya kisarufi, sentensi ya mfano wa matumizi ya kidahizo n.k. Kidahizo pamoja na maelezo yake ndiyo huitwa kitomeo cha kamusi.

Kutafuta Maana Unayoitaka

Neno linaweza kuwa na maana moja au zaidi ya moja. Maana inapokuwa moja, mtumiaji kamusi hana tatizo kwani hiyo ndiyo atakayoipata na kuichukua. Lakini neno linapokuwa na maana zaidi ya moja, mtumiaji kamusi hutatanika asijue ni ipi aichague. Ili kupata maana inayosadifu, inafaa mtumiaji kamusi kutafuta maana ambayo inahusiana na muktadha wa neno linalotafutwa.

Mfano:

kifungo nm vi-

  1. kitu cha kufungia
  2. kitu kinachotumiwa kufungia vazi kama vile shati, gauni, suruali n.k
  3. adhabu ya mtu kuwekwa jela kwa muda fulani

Iwapo mtumiaji aliona neno ‘kifungo’ kwa muktadha wa: “Juma alihukumiwa kifungo cha miaka kumi baada ya kupatikana na hatia ya kubaka….” Maana ya muktadha huu itakuwa ni ile maana ya 3 kwa sababu ndiyo yenye kuhusiana na muktadha ambapo neno kifungo limetumika na wala siyo maana ya 1 wala ya 2.

Leave a Comment


Share this Doc

Ufahamu

Or copy link

CONTENTS

Translation And Interpretation | English Form 5 & 6

Translation is a process by which ideas that are written in one language ar...

Writing Skills | English Form 5 & 6

Are the abilities that allow you to write effectively and concisely. A competent...

Reading Skills | English Form 5 & 6

Reading is the process of going through written information or piece of wor...

Speaking Skills | English Form 5 & 6

What is Speaking? SPEAKING SKILLS: Speaking is simply the act of talking wh...

Listening Skills | English Form 5 & 6

Listening is ability to accurately receive and interpret messages in the communi...

Word Formation | English Form 5 & 6

This is the field or branch of morphology which studies different principles or ...

Introduction To Language | English Form 5 & 6

Language is a symbol system based on pure or arbitrary  conventions…...

Topic

Form Five and Form Six

Ecology

Ecology is the study of the interactions between living things, such as humans, ...

Evolution

EVOLUTION Evolution is  a change in the genetic composition of a population...

Genetics

Genetics is the study of heredity and variationHeredity- is the passage of chara...

Chat Icon Close Icon

Subscribe

×
Cancel